Hebrews 5

1 aKwa maana kila kuhani mkuu anayechaguliwa miongoni mwa wanadamu anawekwa kuwawakilisha kwa mambo yanayomhusu Mungu, ili apate kutoa matoleo na dhabihu kwa ajili ya dhambi. 2 bKwa kuwa yeye mwenyewe ni dhaifu, aweza kuwachukulia kwa upole wale wasiojua na kupotoka. 3 cHii ndiyo sababu inampasa kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe na vivyo hivyo kwa ajili ya dhambi za watu. 4 dHakuna anayejitwalia heshima hii mwenyewe; ni lazima aitwe na Mungu, kama vile Haruni alivyoitwa. 5 ePia Al-Masihi hakujitwalia utukufu yeye mwenyewe wa kuwa Kuhani Mkuu, bali Mungu alimwambia, “Wewe ni Mwanangu;
leo mimi nimekuzaa.”

6 fPia mahali pengine asema, “Wewe ni kuhani milele,
kwa mfano wa Melkizedeki.”

7 gKatika siku za maisha ya Isa hapa duniani, alimtolea maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, yeye awezaye kumwokoa na mauti, naye Mungu akamsikia kwa sababu ya kutii kwake kwa unyenyekevu. 8 hIngawa alikuwa Mwana, alijifunza utiifu kutokana na mateso aliyoyapata, 9 ina akiisha kukamilishwa, akawa chanzo cha wokovu wa milele kwa wote wanaomtii. 10 jNaye amewekwa na Mungu kuwa Kuhani Mkuu kwa mfano wa Melkizedeki.

Wito Wa Kukua Kiroho

11 kTunayo mengi ya kusema kuhusu habari ya ukuhani huu, lakini ni vigumu kuyaeleza, kwa sababu ninyi ni wazito wa kuelewa. 12 lKwa hakika, ingawa mpaka wakati huu ingewapasa kuwa walimu, bado mnahitaji mtu wa kuwafundisha tena hatua za awali za kweli ya Neno la Mungu. Mnahitaji maziwa, wala si chakula kigumu! 13 mKwa maana yeyote aishiye kwa kunywa maziwa bado yeye ni mtoto mchanga, hana ujuzi katika mafundisho kuhusu neno la haki. 14 nLakini chakula kigumu ni kwa ajili ya watu wazima, ambao kwa kujizoeza wamejifunza kupambanua kati ya mema na mabaya.
Copyright information for SwhKC